JIFUNZE KUSAMAHE EWE MKRISTO




Na; Frt  Peter  Mwikwabe
“Utusamehe makosa yetu kama tunavyowasamehe na sisi waliotukosea”
[Mathayo 6:12]
Msamaha ni hali ya kuachilia maumizo na makwazo uliyotendewa na kuacha moyo wako kuwa huru na kusahau yaliyopita. Msamaha ni kanuni ya maisha, Mungu alipotuumba katika ubinadamu wetu alituwekea kanuni ya lazima yaani kusamehe. Matokeo ya kushindwa kuifuata kanuni hii ni kutosamehe ambako kunatutesa tulio wengi. Msamaha ni hitaji lililositizwa kwa kiasi kikubwa katika neno la Mungu, soma vifungu vifuatavyo, Kolos  3:8-9, Mt 18;21-34, Mk 14;66-72, Efe 4;31-32, Mt 6;15, Lk 6;36, Mt 5;23-24, Rum 12;17-21, Ebr 8;12, Luk 6:27-28, 1Sam 25:1-37, Mdo 6;8-10, 7;54-60, Zab 51:1-19, Mith 19;11, Sira 28;1-3, Law 19;17-18, Luka 23;34.
Swali. Je, tunaweza kusamehe na kusahau ?Jibu nindiyo, ni kweli wanadamu tumepewa uwezo wa kukumbuka tena mambo mengi tu. Tunaposema kusamehe na kusahau maana yake ni kwamba, ukishamsamehe mtu aliyekuumiza hata kama utaendelea kukumbuka na kuhisi kinyongounapaswa kuachia maumizo yote na usiendelee kuliongelea jambo lililokuumiza, kwani kufanya hivyo ni kutonesha kidonda. Kumbukumbu za maumivu zitakuwepo kwa sababu ni ubinadamu lakini jiachie kwa Bwana Yesu atakusaidia na taratibu utasahau, lakini usimwambie mtu nimekusamehe lakini sitakusahau, hapo utakuwa bado haujaanza mchakato wa kusamehe. Unaposamehe na kusahau unafungua ukurasa mpya wa maisha na hakuna kurudi nyuma, ni kama vile ukishatapika hakuna kuyarudia yale matapishi huko ndiko kusamehe na kusahau.
Msamaha unaponya, Daktari Louis Hay katika kitbu chake cha You can heal your life [unaweza kuponya maisha yako] anasema kuwa, asilimia kubwa ya magonjwa ya binadamu yanatokana na hali yetu ya kushindwa kusamehe. Ni kweli kabisa magonjwa mengi tuliyonayo binadamu ni kwa sababu ya kushindwa kusamehe. Tukumbuke kuwa unaposhindwa kufungua moyo na kusamehe unatengeneza sumu mwilini mwako bila wewe kujua, kwa watu wengi wanaotawaliwa na hasira huwa wanajipungizia muda wa kuishi, wataaalamu wa afya wanasema kuwa unapokasirika mwili unatumia nguvu nyingi ambazo zilibidi zitumike kwa ajili ya kusukuma damu, kufanya mmeng’enyo wa chakula na kuendesha mifumo mingine ya kimwili. Unapokasirika unavuruga mifumo hiyo inayoongoza mwilina hivyo kujisababishia maradhi kama ya kansa, vidonda vya tumbo, maumivu ya uti wa mgongo, presha, kisukari, TB nk. Ili kuthibitisha hili mwaka 2009 wataalamu wa afya kule Bangalore nchini India walifanya utafiti na kusema kuwa, kwa wagonjwa wengi maumivu makali ya uti wa mgongo hutokana na hali ya kushindwa kusamehe.

AINA ZA MSAMAHA
Msamahaumegawanyika katika makundi makuu manne  yote yana lengo la kuleta Amani na uponyaji.
(a)    Kujisamehe mwenyewe
(b)   Kumsamehe Mungu
(c)    Kusamehe tetesi
(d)   Kusamehe wengine

Kujisamehe mwenyewe
Katika kuanza mchakato wa kusamehe ni vema kwanza kutambaua umuhimu wa kujisamehe, yaani kujifariji, kujiwazia mawazo mazuri, kujipenda na kujithamini. Wengi tunashindwa kusamehe kwa sababu bado hatujajisamehe tumebeba majeraha moyoni na wala hatujiwazii mawazo mema. Unapojisamehe unamuweka huru mfungwa, na utagundua kuwa mfungwa ulikuwa wewe mwenyewe ndani ya gereza la moyo wako. Mungu mwenyewe anasema,nimekupenda kwa upendo wa milele ndio maana nimekuvuta kwa fadhili zangu [ Yer 31:3], kwa hiyo una kila sababu ya kujjipenda na kujisamehe kwa sababu hata Mungu anakupenda kuliko unavyofikiri, sikiliza anavyosema kupitia neno lake
Je, mwanamke anaweza kumsahau mtoto wake anyonyaye.
Hata asimhurumie mwana wa tumbo lake?
Naam hawa waweza kusahau,
Lakini mimi sitakusahau wewe.
Tazama nimekuchora kwenye viganja vya mikono yangu,
Kuta zako ziko mbele yangu daima. [ Isaya 49:15-16]
Utafiti uliofanywa na chuo kikuu cha Havard Marekani ulitoa ujumbe huu, ukitaka kuwa na Afya njema, kuishi muda mrefu pasipo msongo wa mawazo na mfadhaiko ni lazima kujenga utamaduni wa kuachilia maumivu ya zamani na kusamehe.
Msamehe Mungu
Wakati mwingine Mungu huamua kutupitisha katika changamoto na magumu mbalimbali ya maisha kwa mfano Ayubu. Lengo la kufanya hivi ni kuimarisha Imani yetu hata Bwana Yesu alipitishwa kwenye mateso. Nyakati kama hizi tunapaswa kuwa wanyenyekevu na kupokea mapenzi ya Mungu kwa moyo mkunjufu, kwa mfano mama Hellen Keller aliyekuwa mwandishi wa vitabu vya kutia moyo na kuleta matumaini huko nchini Marekani, alipatwa na matatizo makubwa ya kiafya hali iliyompelekea kupoteza uwezo wa kusikia lakini yeye alimsamehe Mungu kwa kuyapokea mateso kwa moyo mkunjufu, hata alipoulizwa ungependa Mungu akutendee nini, yeye alijibu ningepenada Mungu atujalie sisi sote kuishi kwa Amani, Tumsamehe Mungu kwa kuruhusu mateso yatupate [Ebr 12:4-7]. Ayubu pia alimsamehe Mungu kwa kuyapokea mateso yake kwa moyo wa matumaini, Ayubu alisema ikiwa tumepokea mema toka kwa Mungu kwa nini tusipokee na mabaya. Ayubu aliendelea kuweka matumaini yake kwa Mungu lakini yeye aijua njia niendeayo, akisha kunijaribu nitatoka kama dhahabu [Ayub 23;10]
Kusamehe tetesi zote
Maishani tunakumbana na tetesi na maneno mengi, mengine ya kukatisha tamaa na kuvunja mioyo, samehe tetesi zote, samehe maneno yote mabaya yaliyonenwa juu yako, samehe maneno ya chuki, dharau na kejeli yaliyosemwa dhidi yako. Mtazame Yesu kristu aliyesemwa vibaya na kutukanwakila aina ya matusi lakini alisamehe  na wala hakukata tamaa. Yesu kristu aliitwa mlafi na mlevi [Luka 7:34], aliitwa mwendawazimu [Marko 3:21], aliitwa mkiuka mila [Luka 11;45], aliitwa mtoa maneno ya kufuru [Luka 5;21] na wengine walimuita mjinga,lakini alisamehe yote. Je, mimi na wewe tuko tayari kuiga mfano wake? Abrahamu Lincoln raisi wa 16 wa Marekani alikuwa na wapinzani wengi waliokuwa wakimkosoa vibaya na alipoulizwa ni kwanini hapendi kuwaadhibu hao madui zake, yeye alikuwa na haya ya kusema juu ya hao wapizani wake ninawaangamiza maadui zangu kwa kuwasamehe na kuwafanya marafiki
          Samehe wengine
Bwana Yesu alitufundisha kupitia kwa mtume Petro kusamehe saba mara sabini yaani kusamehe bila mipaka. Msamehe jirani yako, msamahe mwenzi wako wa ndoa, msamehe mtawa mwenzako, wasamehe marafiki zako, wasamehe viongozi wako na wasamehe ndugu zako pia, mfano mzuri ni Yosefu wa agano la kale aliyeuzwa na ndugu zake utumwani,lakini alikuwa tayari kusamehe na kuwasaidia hao ndugu zake licha ya kwamba walimtendea jambo baya sana kibinadamu. Biblia inatuambia tafuteni kwa bidii kuwa na Amani na watu wote na huo utakatifu hakuna mtu atakayemuona baba asipokuwa nao [Ebr 12:14].   Kusamehe wengine na kijsamehe mwenyewe ni tiba tena ya magonjwa sugu. Nimewahi kumsikiliza Bwana mmoja aliyepona ugonjwa wa moyo baada ya kukubali kumsamehe bosi wake aliyemdhulumu mshahara wake.
          JINSI YA KUSAMEHE NA KUSAHAU
i.                    Omba neema ya Mungu kwa njia ya sala kwa sababu msamaha ni tendo la kiroho na wala sio rahisi kulifanya kibinadamu
ii.                  Kataa kuongozwa na Hasira: muwe na hasira lakini msitende dhambi, Jua lisichwe na uchungu wenu bado haujawatoka wala msipe ibilisi nafasi [Efe 4;26-27]
iii.                Tafuta mtu mwenye busara anayeweza kuwa mshauri wako hasa katika nyakati ngumu zenye ugumu wa kuachilia maumivu, unaweza ukawaona hata viongozi wako wa dini
iv.                 Jenga utamaduni wa kujishusha, uwe mnyenyekevu
v.                   Usiweke makwazo moyoni mwako, yakija yapokee kama kitu cha kawaida wala usipaniki
vi.                 Tambua madhara ya kutosamehe
vii.               Tamadunisha maisha ya upendo
viii.             Tambua usiposamehe nawe hautasamehewa na wala sala yako haitajibiwa
ix.                Tumia msaada wa neno la Mungu [Biblia] mtume Paulo anasema neno la Mungu na likae kwa wingi mioyoni mwenu [kolos 3;16]
x.                  Uwe mvumilivu, sio kitu kidogo tu unajaa uchungu moyoni


Tuombe neema ya Mungu atujalie nguvu na uthabiti wa  kutoa na kupokea msamaha, ingawa ni kweli kabisa kuwa neno hili samehe kwa tulio wengi ni neno gumu na zito kwa sababu tumejeruhiwa sana na wenzetu. Ukiwa katika hali hiyo fungua moyo wako na ukamkaribishe Bwana YESU naye atakusaidia.

MASHUJAA WALIOTOA  MSAMAHA

Nelson Mandela [1918-2013], Hayati mzee Nelson Mandela alifungwa gerezanikwa miaka 27 bila kuwa na hatia yoyote. Humo gerezani aliteswa na kupata manyanyaso ya kila aina toka kwa makaburu. Lakini baada ya kuachwa huru na kutangazwa kuwa raisi naye akatangaza msamaha kwa watesi wake ingawa alikuwa na uwezo wa kulipa kisasi. Baada ya kutoka grezani alisamehe na kusema kuwa, Nilivyotembea kutoka mlangoni na kuelekea lango ambalo nilikuwa natokea na kwenda kwenye uhuru wangu, nilijua kama nisingeacha ukali wangu na chuki nyuma yangu, ningeendelea kuwa mfungwa. Mandela aliwahi pia kusema kuwa, Watu wenye ujasiri hawaogopi kusamehe kwa ajili ya Amani

Mt. Papa Yohani Paulo II [1920-2005], Huyu anajulikana pia kama mwanariadha wa Mungu kwa sababu ya bidii yake ya kueneza injili ya Kristo Duniani, Siku ya tarehe 13 May 1981  Papa Yohani Paulo wa pili alipokuwa akihutubia watu kwenye viunga vya Mt. Petro vatican alipigwa risasi kali ambazo nusura zikatishe uhai wake, baada ya kukimbizwa hospitali kwa matibabu na kupata nafuu alimsamehe kijana Mehmet Ali Agca aliyemfanyia hayo madhara na alikwenda gerezani kumtembelea na kuzungumza nae.

Mt. Josephina Bakhita [1869-1947], Tunapenda kumuita mtumwa aliyekutana na kristoBakhita aliteswa sana utumwani na kuachiwa alama za minyororo na makovu yapatayo 144 mwilini mwake baada ya kukatwakatwa kwa kisu kikali na kisha vidonda vile vikapakwa chumvi. Hebu fikiri Bakhita alipata uchungu na maumivu makali kiasi gani? Pamoja na maumivu yote aliyopataBakhita alifungua moyo wake kwa Yesu Kristu na kutangaza msamaha kwa watesi wake kwa maneno haya: nimewasamehe wote walionitesa utumwani na kama ningekutana nao ningewabusu miguu, kwa sababu pasipo wao kunitesa kwa mateso makali nisingemjua kristo.
Mashujaa wengine ni kama Stephano [ Mdo 6;8-10,7;54-60 ] na Martin Luther King [1929-1968], yeye pia aliwasamehe maadui zake waliokuwa wanapinga juhudi zake za kutetea haki za wanyonge, alitufundisha kuwa Chuki haiwezi kuondoa chuki ni upendo pekee unaoweza kufanya hivyona aliuawa kwa sababu ya chuki za watu.

Hitimisho,Unaposoma au kusikia ujumbe huu ni vema mimi na wewe tukajitafiti maisha yetu tuone ni wapi mahusiano yetu na wenzetu yameharibika na kisha tuchukue hatua za kuanza mchakato wa kuleta Amani na maridhiano.
Utambulisho wa mkristo ni upendo na utambulisho wa upendo ni msamaha. Je, mimi na wewe tuko tayari kutoa na kupokea msamaha?Papa Francis alitufundisha kuwa,msamaha huleta furaha pale uchungu ulipoleta maumivu, huleta uponyaji pale uchungu ulipoleta magonjwa..

Mungu wetu ni mpole na mwenye huruma [Luka 1;78]

Tumsifu Yesu kristu………………………


Imendaliwa na: Frt Peter  Mwikwabe, wa Shirika la Mateso ya Yesu kristu [wapasionisti]toka seminari kuu ya Falsafa ya Roho mtakatifu-Arusha [Spiritan Missionary Seminary].
Makala hii imeandaliwa kwa msaada wa vitabu vya You are not Rejected, Huruma ya Mungu ni kwa watu wote, We are more than conquerors,Matatizo ni daraja, Biblia takatifu na taarifa mbalimbali za mtandaoni.
0757724342
Email: petermwikwabe20@gmail.com

Comments