Na Rodrick Minja, Dodoma
Waamini
wa Kanisa Katoliki nchini wameaswa kufahamu kuwa mafuta Matakatifu ya Krisma yalitokana na Utakatifu wa Kristo na
hivyo kupewa jina hilo ili kuleta ukombozi kwa wale wote waliozaliwa mara ya
pili.
Hayo
yamebainishwa na Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Dodoma Mhashamu Beatus Kinyaiya wakati wa ibada ya misa
takatifu ya kubariki mafuta ya krisma iliyofanyika katika Kanisa la Mtakatifu Paulo wa Msalaba
Jimboni hapa.
Askofu
Mkuu Kinyaiya amesema kuwa katika maisha yetu tunapaswa kuwa watu wenye kutenda
matendo ya huruma kwani Mwenyezi Mungu amefanya hivyo kwa upendo usio na kifani
kwa ajili ya kutuandalia mkombozi ambaye aliteswa, akafa na hatimaye akafufuka
siku ya tatu kwa ajili ya kutukomboa sisi wanadamu kutoka katika lindi la
dhambi.
Hata
hivyo amesema kuwa sisi ni wanadamu ambao ni wakosaji na wenye dhambi hivyo ni
muhimu kujitafakari kwa kina na baada ya hapo tujue haya tunayoyafanya tunayafanya
kwa nguvu za nani na hata kama ni sifa tunapewa tunapaswa kuzitafakari sifa
hizo kama tunastahili kuzipokea.
“Alikuwepo
Padri mmoja ambaye alikuwa ni muhubiri mzuri na hodari wa kutoa mahubiri yaliyo
mema na mazuri kwa waamini lakini alikuwa mara baada ya ibada anatoka nje na
kuanza kujisifia kwa waamini kuwa mmesikia vigongo nilivyotoa kwenye mahubiri?,
sasa tujiulize tusisahau tunafanya kwa urahisi na kupata sifa nyingi je
aliyetuwezesha tunamkumbuka?” aliongeza Askofu Mkuu Kinyaiya.
Kwa
upande wa mapadri, Askofu mkuu Kinyaiya amewataka mapadri kutumia tunu, karama
na vipaji walivyojaliwa na Mwenyezi Mungu katika kulikuza shamba lake na siyo kinyume na hapo.
Askofu Mkuu Kinyaiya alisema kuwa wapo baadhi ya Mapadri wamekuwa wakitumia vipaji na
tunu walizojaliwa kinyume na mapenzi ya mungu hivyo kuwataka kubadilika .
“
Tunu, karama na tunu mlizojaliwa zisiwape kiburi, Mwenyezi Mungu kawawezesha
hivyo mshukuruni kwa kuwawezesha kwa yote mlionayo” aliongeza Askofu Mkuu
Kinyaiya.
Pia
amewataka kutokukubali kuruhusu kishawishi chochote kile amabacho kitawapelekea
kukengeuka na kuanguka katika njia yao iliyo nzuri na badala yake kuwataka
kusimama kidete katika kulihubiri neno la Mungu na katika utume wao.
Kuhusiana
na wito waliouchagua, Askofu Mkuu Kinyaiya amewataka kujenga upendo baina yao
kama bwana wetu Yesu Kristo alivyosema kuwa amri kuu nawapeni ni upendo
Pendaneni kama nilivyowapenda ninyi.
Hata
hivyo amewataka mapadri kuhakikisha wanapokutana katika dekania zao wajenge
kasumba ya kuendesha ibada ya misa kabla ya mikutano yao na kuwataka mapadri
wote wanaofanya kazi za utume katika Jimbo kuu Katoliki Dodoma kuhudhuria
mikutano hiyo kwani mikutano hiyo ya dekania sio maalumu kwa mapadri wa
Dekania pekee bali ni kwa mapadri wote waliopo katika Jimbo Mahalia.
Askofu Mkuu Kinyaiya pia amezitaka Parokia Dada kukaa na kuangalia ni kwa namna gani
wanaweza kusaidiana ili kusongesha mbele gurudumu la utume katika Jimbo Kuu
Katoliki Dodoma.
Askofu
Mkuu Kinyaiya amesema kuwa mapadreiwana wajibu wa kushirikiana katika kila
jambo na kuweka mbali tofauti zao za kidekania ili kuweza kusimamia vyema
kondoo zao na hatimaye kujenga mahusiano mazuri baina yao na waamini wao kwa
kutengeneza mazingira ya kutembeleana hata katika vituo vyao wanavyofanyia
utume.
Kuhusu
utoaji wa Sakramenti ya Kitubio amewashauri mapadri kuwa wanabadilishana wa
parokia hii anakwenda parokia ya mwenzake kwa ajili ya kutoa sakrtamenti ya
kitubio kwani wengi wa waamini wanashindwa kushiriki sakramenti hiyo kutokana
na mazoea na ukaribu au kumfahamu anayemuungamisha .
Katika
ibada hiyo ya kubariki mafuta ya Krisma pia mapadri wamerejea viapo vyao vya
utii kwa Askofu mbele ya Baba Askofu
mkuu na mbele ya waamini wote waliohudhuria katika ibada ya misa takatifu.
Hata
hivyo, Askofu Mkuu Kinyaiya amehitimisha kwa kuwapongeza waamini kwa
utulivu wao katika parokia walizopo na pia amewataka mapadri kuhakikisha kuwa
wanazitafutia suluhu ndoa zenye migogoro na changamoto mbalimbali.
Aidha
Mafuta yaliyobarikiwa leo hii ni pamoja na Mafuta ya krisma ambayo hutumika
kutabaruku Kanisa, Altare, kumweka wakfu Padri na Askofu, huku mafuta ya
wakatekumeni yakitumika katika kuwabatiza wakatekumeni na mafuta ya wagonjwa
yakitumika kuwapaka ili kuwapa faraja.

Comments
Post a Comment