TUMWOMBEE RAIS WETU MAGUFULI-ASKOFU NGALALEKUMTWA

Na Getrude Madembwe, Iringa.

Askofu wa Jimbo Katoliki Iringa Mhashamu Tarcisius Ngalalekumtwa amewataka waamini kumuombea Rais wa Tanzania Dkt. John Magufuli na serikali yake ili waweze kuliongoza Taifa kwa haki na Amani.

Aidha  amewataka pia waamini hao kuombea hali njema ya hewa ili mazao yaliyo mashambani yaweze kustawi vizuri sababu mazao mengine bado madogo na yanahitaji mvua.

Askofu Ngalalekumtwa ameyasema hayo wakati wa homilia yake kwenye misa takatifu ya Pasaka katika Kanisa Kuu la Moyo Mt. wa Yesu Parokia ya Kihesa na kuhudhuriwa na watawa kutoka mashirika mbaimbali yaliyopo jimboni hapa na waamini wenye mapenzi mema.

“ Amani tuliyonayo ni tunu kutoka kwa Mungu hivyo watanzania tunapasika kuilinda, tumuombee pia Rais wetu na serikali yake ili iwe yenye huruma na inayoongoza kwa kufuata msingi ya haki.” amesema mhashamu Ngalalekumtwa.

Mhashamu Ngalalekumtwa amesema kuwa, pasaka ni karamu ya upole, wema ni kuhama kutoka penye hali mbaya ya kuwa mnyonge ili waweze kuishi mbali na utumwa wa ibilisi.

“Pasaka hii inatufundisha kutendeana mema, wema kwamba tunapoadhimisha pasaka watafute haki, watafute Amani kwa kila mmoja wetu atambue na aone kuwa mwenzake anastahili kulindwa na kutendewa haki ma kusaidiwa kukuza karama zile alizojaliwa na Mungu, wadogo na wanyonge wapewe upendeleo katika akili zao na ndipo Mungu wetu atakapotukumbatia ikiwa watawakumbatia wanyonge na wenye shida.” amesema Askofu  Ngalalekumtwa.

Amewataka waamini hapo pia kuombea ustawi wa Imani yao na hasa kwa kipindi hiki wanapomshukuru Mungu na kuelekea kuadhimisha miaka 150 ili ionekane miaka hiyo imewapeleka pazuri

“Tunasema miaka 150 ya uinjilishaji, tujiulize miaka 200 iliyopita ilikuwaje, kama tulijaliwa na ukweli wa injili tuikumbatie tusiwe kama walivyoishi wengine, haitoshi kuwa na majina ya kikristo kinachotakiwa ni unyenyekevu ndani ya moyo, waishi maisha mazuri yenye upole, utulivu na Amani ili wajazwe tumaini jipya na wokovu.” amesisitiza Askofu Ngalalekumtwa.

Comments